ONGEZEKO LA AJIRA 01/02/2016

WATUMISHI WA SEKRETARIETI YA AJIRA WAMETAKIWA KUONGEZA KASI NA UFANISI KATIKA KUENDESHA MCHAKATO WA AJIRA NCHINI

Watumishi wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma wametakiwa kuongeza kasi katika kuendesha mchakato wa ajira pamoja na kuzingatia maadili katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.
Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma Dkt. Laurean Ndumbaro amesema hayo wakati alipotembelea Ofisi za Sekretarieti ya Ajira na kukutana na  Menejimenti  pamoja na Watumishi wa ofisi hiyo ili kujifunza na kujionea namna Sekretarieti ya Ajira inavyofanya kazi katika kutimiza majukumu iliyokabidhiwa.
“Ni vyema mkafanya kazi kwa kasi zaidi ili siku za kuendesha mchakato wa ajira zipungue, na pia ni muhimu kuendelea kufuata maadili ya kazi kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu ili mtu anayeajiriwa awe ni yule mwenye sifa na vigezo stahili na si vinginevyo” alisisitiza Dkt. Ndumbaro.
Aliongeza kuwa endapo watumishi watazingatia maadili ya Utumishi wa Umma ipasavyo basi malalamiko ya upendeleo kutoka kwa wadau  yanaweza kupungua kama sio kuisha kabisa kwa kuwa anatambua fursa za ajira ni chache na kila mwombaji angependa kupata fursa.
Mbali na hayo alihimiza juu ya umuhimu wa kuwa na vikao vya pamoja baina Idara, Vitengo na Menejimenti kukutana kwa pamoja kila mara ili kufanya kazi kwa ushikiano zaidi, kwa kuwa kila mtumishi atakuwa anafahamu kinachoendelea ndani ya taasisi na mikakati iliyopo  kwa lengo la kuimarisha utendaji na kuongeza ufanisi.
Aidha, Katibu Mkuu huyo aliweza kupata maelezo ya kina ya namna majukumu ya mchakato wa ajira yanavyotekelezwa na ofisi hiyo pamoja na kujionea hatua kwa hatua namna mfumo wa kupokea maombi ya kazi kwa njia ya Kielektroniki unavyofanya kazi kuanzia tangazo la kazi linapotolewa, mwombaji wa fursa za ajira anavyojisajili na kuwasilisha maombi yake ya kazi na taratibu nyingine zinavyofanyika hadi mchakato mzima wa ajira kukamilika. 
Ndumbaro  alipongeza matumizi ya mfumo wa kielektroniki unaotumiwa na taasisi hiyo kwa kuwa umeweza kusaidia kupunguza baadhi ya malalamiko hususani ya kupotea kwa maombi ya kazi. 
Aidha, alisema amepokea changamoto ambazo Sekretarieti ya Ajira inakabiliana nazo na kuahidi kuangalia namna atakavyoweza kushirikiana na taasisi hiyo katika kukabiliana nazo ili chombo hicho kiweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi zaidi. 
Kwa upande wake, Katibu wa Sekretarieti ya Ajira, Bw. Xavier Daudi mbali na kutoa ufafanuzi wa namna chombo hicho kinavyofanya kazi, alimshukuru Katibu Mkuu huyo kwa kuwatembelea na kuahidi utendaji wenye tija zaidi ili kukidhi malengo.
Imetolewa na kitengo cha mawasiliano Tanzania.
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
29 Januari, 2016